Wednesday, June 20, 2012

Sababu za wanawake kuandamwa na chunusi

TATIZO la chunusi, linawasumbua wengi wanawake sana hadi baadhi yao kufikia hatua ya kukata tamaa kutokana na kukosa ufumbuzi wa kudumu wa tatizo hilo.

Je, unaelewa kuwa kwa asilimia 99, chunusi kwa mwanamke husababishwa na yeye mwenyewe?
Mambo yanayosababisha chunusi kwa mwanamke ni haya yafuatyo:

Ulaji usio makini: Wakati mwingine ulaji wa vyakula vyenye mafuta humweka mlaji hususani mwenye ngozi ya mafuta kupata chunusi. Si hivyo tu, wakati mwingine kutokula chakula bora kunaweza kukuletea tatizo hilo.

Matumizi ya nguo chafu: Kulala kwenye foronya chafu zenye vumbi na mafuta pia hukuweka kwenye hatari ya kupata chunusi, ni vyema hili likatambuliwa na kila mwanamke.

Unashauriwa kuvaa kofia ya kulalia wakati wa kulala ili kuepuka kuchafua foronya zako, na pia kufanya usafi wa mara kwa mara wa foronya na shuka za kulalia.

Kujishika usoni mara kwa mara: Wanawake wengi wanapenda kujishika usoni mara mwa mara, bila kuwa na hawana uhakika na usafi wa mikono yao. Jambo hili mara kadhaa limekuwa likisababisha, maambukizo ya bakteria katika ngozi wanaoleta maradhi kama vile ya chunusi na mengineyo.

Kuzembea wakati wa kuosha nywele: Kwa kawaida vipodozi vya nywele huambatana na mafuta wingi. Hivyo mhusika asipokuwa makini wakati wa kuosha, wakati mwingine husababisha mabaki ya mafuta hayo kuingia usoni na hivyo kuiweka ngozi ya uso katika hatari ya kupata chunusi.

Matumizi yasiyofaa ya vipodozi: Kutumia vipodozi bila kufuata ushauri wa wataalamu, husababisha wahusika kuzalisha chunusi. Kwa mfano mwenye ngozi ya mafuta anapotumia vipodozi vya mafuta husababisha kutokea kwa chunusi.

Ukosefu wa elimu ya utunzaji wa ngozi: Kila ngozi ya mwanamke inatakiwa kufanyiwa huduma mbalimbali kama vile scrub, kuondoa seli zilizokufa, kuwekewa mvuke na nyingine nyingi. Wakati mwingine ikiwa haya hayakufanyika , huwa ni chanzo cha uzalishaji wa chunusi katika ngozi.

Kulala na vipodozi: Hili ni tatizo sugu kwa wanawake wengi. Wengi kutokana na hali fulani hushindwa kuondoa vipodozi wakati wa kulala hivyo kujiweka kwenye hatari ya kupata chunusi. Hakikisha unaondoa vipodozi vyote kabla ya kwenda kulala.